HII ni kwadresma, waumini wa Kikatoliki wanafahamu kipindi hiki sana. Kipindi cha kugeuza shavu la kushoto pale upigwapo la kulia. Kipindi cha kumkumbuka huyu Mwanafalsafa aliyepewa jina la Yesu. Huyu jamaa kama aandikavyo Profesa Kezilahabi katika "Nagona" ananiathiri sana katika maisha yangu. Natamani nami nikifa kifo kama chake. Kifo cha jamii kukuita mshindi huku ukijitazama. Kifo cha umma kukutangaza mfalme wakati wako wa kumaliza maisha. Kifo cha kuwatazama wanaokulilia na kukucheka! Kifo hiki ndicho hasa niombacho nami nipewe lakini wana heri wasiotamani kutaka kujifananisha na Masiha. Yeye alishajua kuwa nitaandika hapa leo. Anajua kuwa ninaomba kifo kama chake lakini anataka kazi ndogo tu, kujikana na kushika njia yangu. Anataka kujua kama unatumia nafasi yako kuwanufaisha wengine. Anataka mengi madogo madogo tu. Nisitamke sana picha hii inisemee, iamshe fikra mpya katika mapambano ya kiuchumi Afrika. Itoe fikra mpya ya kuandika barua yangu kwa mama.
Uongozi wa mwanafalsafa Yesu ni maneno mengine kabisa, huyu ndiye aliyewapenda watu wake kwa moyo wake wote, hakutaka makuu wala kujipendelea. Pengine kuna haja ya kuanza kumtizama Yesu katika mtazamo usio wa kidini, hii itasaidia watu kumtafakari na kuzifuata nyayo zake pasipo migogoro yoyote. Ninaamini watu wengi wanashindwa kuzifuata nyayo za kiongozi Yesu kwa vile wamemuweka katika kundi la dini ambazo nazo zimejaa migogoro mitupu. Naomba kutoa kauli yangu Yesu/Issa/Joshua hakuja kutuletea dini bali alikuja kutufundisha uongozi mwema na wa haki, Uongozi wa kujikana mwenyewe. Na kama tukiufuata uongozi wa namna yake basi haya matatizo madogomadogo ya kupelekana mahakama ya 'The Hague' hayatapata mwanya.