Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Thursday, March 02, 2006
JE UMESHAOA MZUNGU?

HAPA Texas sasa ni kipindi cha kampeni za uchaguzi wa awali kabisa. Gharama zake ni kubwa maana hata Mbowe hafiki na Herikopta lake katika chaguzi hizi. Kwa Tanzania chaguzi nkama hizi ni zile za vitongoji, lakini huku wagombea nao hununua matangazo katika Televisheni na mmoja juzi aliniacha hoi alipokuwa akitumia ndege kabisa kupeperusha bango lake. Huu ni utamu kabisa hasa kwetu vichaa wa siasa.

Tumepata bahati ya kutembelewa na wabunge wa Texas mara kwa mara katika madarasa yangu. Humo nashukuru sibaguliwi maana kila mgeni akifika Profesa wangu anamtambulisha kwangu na kumueleza kuwa natoka Tanzania. Anampa walau picha ya kujitahidi kuweka mawazo ya kimataifa ili nami niambulie jambo. Mwisho unakuwa muda wa sisi kuwatwanga maswali. Nimewatwanga maswali kisawasawa na moja kubwa ni mafunzo ya aina ya siasa zinazotakiwa kufanyika. Kama unataka kuwa mwanasiasa unatakiwa kutafuta darasa hili. Baragumu anazo taarifa juu ya nini ukifanye na hii naitamka ili yakitokea mambo kinyume na matarajio yangu, basi muoneni Baragumu atawafafanulia!

Kibaya zaidi ni kila ninapopita katika kona ya barua zangu za mtandaoni. Nakutana na barua ya kijana wa sekondari moja toka eneo lenye ukame wa maji na njaa aliyeweza kufika katika intaneti na kupata wasaa wa kuniandikia waraka. Huyu kajituma kweli maana kipindi hiki chenye umeme wa mgao mtu kufika katika mtandao kunataka moyo kama unabisha muulize MIRUKO atakueleza! Kibaya na kinachonikera ni huyu kijana mbichi kabisa anayepaswa kuwazia masomo kuamua kuvuka nafasi ya mipaka ya nidhamu ya Afrika kwa kuniomba nimtafutie mchumba wa kizungu? Hivi hao mabinti waliojaa hapo Tanzania hamuwaoni? Kama mnashiriki kuwachukia dada zenu kiasi hiki nani atawapenda? Huyu kijana anawakilisha kundi kubwa linaloamini kuwa kitendo cha kuwa mweupe tayari ni kuukata kimaisha. Fikra hizi za kikoloni bado zinaikabili sana Afrika na kuna kazi kuziondoa.

Natulia, kidogo na kufungua barua nyingine. Hii inatoka kwa binti naye anataka nimtafutie mchumba wa kumuoa lakini awe mzungu! Najiuliza hivi kulikoni hapa? Kama dada zetu nao hawatupendi sisi tutaoa wapi? Ina maana kuna mapigano ya sisi kwa sisi au ni yale ya dhana ya kuchanganya mapenzi na mali? Nani kasema kuwa mzungu ni maana ya kuwa na mali? Kuna kazi hapa...

Wakati haya yakiendelea nakumbuka hadithi za mwalimu wangu nikiwa shule ya msingi. Alinambia, "Soma Makene, mabinti hawa watajilerta wenyewe." SIJUI NAYE ALIWAAMBIA AKINA DADA KUWA WASOME KWA KUWA WANAUME WATAJILETA WENYEWE! Nilifaulu shule ya msingi na kuingia sekondari, huko napo nikaambiwa soma mabinti watajileta. Sikuwaona wakijileta hadi nilipoamua nami kuwatafuta. Upweke wa ughaibuni mkali sana na ndio kisa cha mimi kuandika makala haya yaliyokuwemo kichwani kwangu siku nyingi. Nifanyeje wakati sina jiko na umri unakimbia kwa kasi mpya, nguvu mpya na ari mpya? Nguvu za mwili zinazidi na matamanio yanautesa moyo...nawaza huku kukiwa na hoja za kuchanganya kuhusu maamuzi ya kuheshimu tamaa ya mwili wangu au kuacha nafasi ya umma iniamulie matakwa yanayohusu moyo wangu.

Ok narudi nyuma tena, nikafika Sekondari ya juu na huko binti niliyempenda nilimfata na yeye akanitangazia kuwa ana "Boi Furendi" wake Chuo Kikuu. Nikaona bado hadithi za kusoma kwanza zinatakiwa kuendelezwa. Nilipofika Chuo Kikuu sikuwahi kusikia kuwa kuna binti anajisifu kuwa mimi ni "Boi Furendi" wake kwa kuwa nipo Chuo Kikuu. Nikavuta subira, upweke ukaendelea..

Hapo napo nikaamua kumtongoza binti, bila aibu sasa huyu wa chuo kikuu akanambia kuwa ana "Boi Furendi" wake Marekani. Sijui nani kawaloga hawa mabinti, kama ni kusoma si tayari nipo Chuo Kikuu au mwalimu wangu alimaanisha ni mabinti wa aina ipi watakaonifata. Huenda alimaanisha wale niliowaacha kijijini Sitimbi! Siwawezi tena wale maana hawajui losheni na pafyumu, na enjo fesi. Sababu hii inaweza kuwa chuku lakini hasa nao walishanisahau na kikweli hata majina yao sina sasa. Nikabaki kinywa wazi, siku si haba nikahitimu huko na kuja Marekani sijasikia kuwa kuna mtu ananitajataja kuwa mimi ni boifurend wake kwa kuwa niko Marekani. Zaidi ni hizi barua ninazopokea zinazonitaka kuwatafutia wao waume au mabinti wa kizungu. Hivi kila hatua nakumbana na vipingamizi hivi, kuna swali lingine hili limefika sasa hadi nalichukia. Sidhani kama lina lengo la kiubaguzi lakini kwani mahusiano kati ya mtu wa rangi moja na nyingine yanaihusu jamii katika lipi? Hivi kama ni mke nitakayeamua kuoa mimi anaihusu jamii nini, hawa wanaonitaka kuwatafutia mabinti na waume wa kizungu je nao ni wabaguzi wa rangi au wanataka kuvuka mipaka ya rangi zao? Je kwa nini sasa huyu aniulize bila soni swali hili, JE UMESHAOA MZUNGU?
 
© boniphace Tarehe 3/02/2006 12:07:00 PM | Permalink |


Comments: 17


  • Tarehe 3/02/2006 8:46 PM, Mtoa Maoni: Blogger Fikrathabiti

    Ina maana Makene wale mabinti wa ndanda sekondari,warembo wa complex mkwawa na mamiss wako wa UDSM umewasahau au unataka tuamini kua huna bahati katika hii fani???

    Ninayo mengi ya kusema juu ya mtandao wa wanawake wako lakini naashia hapa kwanza nikisubiri michuzi aweke picha zako ulizokua nao hao mabinti kwenye fuko za coco,kipepeo na land mark hadharani!!!!!!!!!

     
  • Tarehe 3/03/2006 12:27 PM, Mtoa Maoni: Blogger John Mwaipopo

    Makene umelizua hapo kwa fikrathabiti.

    Utando wa mawazo ya kumfananisha mzungu na Mungu wengi wetu bado tunao. Anyway, it's just better to taste the other colour. Kamua baba.

     
  • Tarehe 3/03/2006 1:40 PM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    Nimekamaindi kademu!!!

     
  • Tarehe 3/04/2006 6:15 AM, Mtoa Maoni: Blogger Reggy's

    Ni rangi tu. Sote binadamu.

     
  • Tarehe 3/04/2006 6:30 AM, Mtoa Maoni: Blogger FOSEWERD Initiatives

    maweeee maweeeeee maweeeee Makene!soma kwanza mambo mengine baadaye! watakuja wenyewe! kwani umeishakuwa profesa? bado safari ni ndefu sana!!!! ahu ahu ahu !!! kwa kweli hadithi hii nimeipenda na kimsingi ina pande mbili! ya kwanza ni ile ya mwanafunzi mzuri ambaye yuko motivated na future (haijali kama itakuja au la), mwanafunzi ambaye hutabasamu mara chache sana na mara zote kutafuta njia ya kujikeep busy na kuwa serious. mwanafunzi wa namna hii ambaye hawezi kuaccomodate utani utani na romance kwenye maisha yake mara nyingi si chaguo la kina dada....na huishia kuambiwa kuwa nina boi frendi mahala fulani....na kwakuwa mwanafunzi huyu ni mprotokali hana habari kuwa wake zetu wote tuliwachomoa mikononi mwa watu!! ...kwa njia ya kukoleza!!! mfano huu pia nilikuwa nao mie na chuo kikuu nikawa mserekali wa dhati kiasi sikuwa na muda wa kujimix! mwaka wa mwisho wanafunzi wakitaka kunipa serekali ya chuo kama raisi nikasema subutu!!! basi ndio ikawa wenzangu wakiwa busy kuandaa mgomo mie natumia wasaa huo huo kwenda kumuona muhibu mama mtoto wangu tulikutana 1999 ngoma ikapigwa 2002....makene inawezekana uko kwenye kundi hili na inaweza kuwa soo zaidi ukiwa ni "perfectionist"....you will need to know urself ili uenjoy maisha!!

    kundi la pili ni la maplayers ambao wao hawajaweka tittle ya mke kichwani mwao kila mara wanapojichanganya! wao wakimwona demu huanza kufikiria upande wa kujimingo zaidi..an not as a potential running candidate!! namna hii kuna hatari ya kumwacha mgombea mwenza wako. naamini kabisa katika umri huu unachopaswa kufanya ni kukaa chini na kutafakari kama uliwahi kucome across friends kama marafiki au wachumba flani halafu walionyesha vidalili fulani vya kuita (unajua wenzetu hawa hawaongei kwa kusema - si unamcheki hata da mija?) halafu ukaviignore au alikuwa anakutendea mema kuliko kipimo au kujitolea basi pengine huyo ndio alikuwa mgombea mwenza....chukua wasaa kaa chini ita kumbukumbu zako halafu anzisha mawasiliano!! utashangaa majibu yake!! hapa nilipo kuna jamaa wawili (PhD students) walikuwa wanasuffer the same consequence, lakini nilipowashauri i am tell u waliweza kuwafahamu wagombea wenza wao ambao hawakudhani kuwa walikuwa ndo wenyewe na wote kitaeleweka this year!!

    labda kwa upande wa mwisho ni kwamba u need kuwa ukikutana na mtoto wa kike jaribu zaidi kumfikiria kama mke rather than a girlfriend....while the concept is built hutapata shida kuona mbona wako wengi tu? utajua hili ukiishaspecialise!!!
    karibu kwa ushauri zaidi msaki.mark@gmail.com

     
  • Tarehe 3/04/2006 6:41 AM, Mtoa Maoni: Blogger FOSEWERD Initiatives

    cha msingi nilikuja kulearn kuwa mwanamke hata kama hana bf atakuambia kuwa anaye kwani ni kama kakasoro flani kuwa singo, yaani kimsingi inakuwa kama wewe ndio unakuja kumuokoa hivyo anakuwa kama kajishusha value kwako (hutokea mara nyingi kwa wasichana wadogo wadogo ambao hawajafikiria ndoa)! na kingine ni kuwa akisema hana mana yake unajichukulia kama ushindi wa Kikwete na historia inaonyesha kuwa baada ya hapo utamwona bi!!sijui umenipata? katika vitu ambavyo wanandoa huongea na kucheka sana ni vile vya kufukuziana....maisha yote!!!hata kama anaye lakini level of seriousness hutofautiana...wewe ukiwa karateka mzuri utashangaa ataacha ma benz ya bwana mwaipopo na kitofa chake cha mbezi kukufuata uswazi mwananyamala!!!!! khe khe khe !!!

     
  • Tarehe 3/04/2006 6:47 AM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    samahani kukujazia ukurasa ndio kazi zetu za kujitolea....huyo aliyekuuliza ana hamu ya kuolewa na wewe....nenda naye vizuri, angalia kama anafit kwenye criteria zako kama ndio ongeza mawasiliano and you will know what love is!!yaani kwa ufupi, ameamua kuuvunja ukimya liwalo na liwe! mark

     
  • Tarehe 3/05/2006 2:11 AM, Mtoa Maoni: Blogger Egidio Ndabagoye

    Hata mabo si ya kubeza hata kidogo.Itabidi nipate wasaa zaidi wa kuyasoma

     
  • Tarehe 3/05/2006 6:11 AM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    makene inaelekea mbio zako si za kawa...!! ilikuwaje ukaaswa ukiwa msingi?

     
  • Tarehe 3/05/2006 12:22 PM, Mtoa Maoni: Blogger boniphace

    Mimi nasikiliza kwanza mmalize kisha nitamjibu kuanza kwa Fikra Thabiti maana yeye amesahau pasword ya Blogu yake kiasi kwamba hawezi tena kuweka maandishi huko na kazi yake imekuwa kuchukua ukamanda wa kutoa maoni. Enewei natania ila baadaye nitafika hapa na kufafanua nini kilisababisha kuandika riwaya hii.

     
  • Tarehe 3/07/2006 11:27 PM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    Suala la kuchukua mzungu...suala gumu. labda nijisemee mimi. Mimi hata nikipewa wa bure au kulazimishwa....

     
  • Tarehe 3/09/2006 11:48 AM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    Mzee Ndesanjo usiseme hivyo ya Mungu mengi pana leo na kesho mara mzee mzima ndii!!..tena kwa kuangukia.

     
  • Tarehe 3/10/2006 9:59 AM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    Makene, kweli kalamu zimenolewa huku bloguni. Unajua ujumbe wako hapa na maswali yako ungeweza kuandika au kuelezea kwa staili kavu. Lakini umetumia staili ambayo inaburudisha wakati unaelimika na kupata changamoto. Bloguni huku kuna mengi...tuna watunzi, kwa mfano.

     
  • Tarehe 3/11/2006 10:47 PM, Mtoa Maoni: Blogger Mija Shija Sayi

    Kwa hiyo Makene ndio unataka kutuambia hujawahi kubahatika, yaani ni vipingamizi tuu hadi leo?

     
  • Tarehe 3/12/2006 10:31 PM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    Aisee mimi na mzungu ni bila bila! Siwamaindi kabisa hasa ukizingatia kuwa tunatofautiana nao sana...afu wametutesa sana hawa pimbi kuwaoa ni kama kuasi vile?!

     
  • Tarehe 3/13/2006 5:55 AM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    Kuoa mzungu ni sawa na kumdharau mama yako na dada zako. kama unamuheshimu mama wako hutavuka mipaka.

     
  • Tarehe 3/18/2006 11:27 AM, Mtoa Maoni: Blogger FOSEWERD Initiatives

    Makene tatizo la kuoa wazungu ni kanuni zinazidi mipaka...ninawaona huku...yaani ni kuishi kwenye mstari..na kila utachofanya kinataka maelezo...ni gereza au mateso bila chuki....yaani hata kama utaenda kunywa bia lazima upate ruhusa kwanza...na utapangiwa namba ya bia za kunywa...kimsingi ndio maana utakuta kuna watu wanagangamalaaaa weeee halafu wanaachia ngazi wenyewe....

     
   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved