Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Tuesday, January 17, 2006
NYEMBO KWANI WAITWANI?
KUMEIBUKA mwezi wa ushairi katika Blogu za Kiswahili. Alianza Mkwinda, malenga mkongwe kutoka Pwani ambaye amekuja kuwa tishio katika wanablogu wanaogani tungo za mashairi. Katika pita pita akatokeza MWANDANI naye akaimba hivi. Kama haitoshi Malenga mwingine akazaliwa Zanzibar. Huyu ni MATERU. Mjadala wa MKWINDA ukamkuna NYEMBO, akajibu nami nikachangia kidogo. Sasa NYEMBO kapaa kabisa na utungo katika Blogu yake.
Miongoni wa wanaotajwa na NYEMBO katika majigambo haya ya kishairi tunayotaka yachukue sura mpya katika Blogu ni mimi. Sasa natangaza nami kuingia katika majibizano haya ya kishairi na watani wangu hawa nikianza na NYEMBO. Kumbuka hii si nafasi ya kumfanya HARAKATI asahaulike kwa kuwa aliahidi kukariri shairi moja kwa wiki ahadi ambayo haikutimizwa. Pata sasa shairi hili hapa chini.

Nyembo wewe waitwani, hadi uje malengani
Ni wapi unakeshani, tungo zako karirini
Nani amekunyweshani, sumu tamu mezeani
Waweza huu mchezo, ama waja taniani?

Katu sumu simezani, kitumbua situpani
Siki kwangu asalini, utungo jifunikani
Naweza tupa mpini, kisha jembe limiani
Nambie Malenga Nyembo,waitwani shairini?

Diwani ya Nakuzerwa, itatoka si utani
Hodo hodi ni muswada, DAMBAYA kishirikini
Ewe Malenga Mkwinda, huyu Nyembo atokapi?
Kama naye malengani, jinale anaitwani?

Nahisi kaja kwa tambo, wakongwe kuwatishani
Ushairi ni ulimbo, weledi unaletani
Hauji kama mkumbo, kukukuta ukubwani
Nikali mama tumboni, shairi nililighani!

Tungo tungile zamani, sasa kazi someshani
Mama alinambiani, nilivyoghani tumboni
Huzuni kimtokani, siku hizo kumbukani
Kanileta duniani, njia nachia tambaa.

Nyembo toa masharubu, kama wataka tungani
Utajageuka bubu, ulingoni kimbiani
Tambua huu weajibu, mahoka waulizani
Kama wadhani mchezo, uliza upotokani!

Mwandani nawe changia, uvamizi uwanjani
Beti waweza pangia, Mshairi kuitwani?
Hoja waweza pangia, kisha ngoma alikwani?
Mshairi mtu gani, hoja hii fafanua!

Natoka sasa wagenzi, hoja nimeanikani
Tungo zachie wapenzi, walale wakiliani
Ghani wache wakufunzi, walale wasibaini
Kisha Nyembo rudi tena, kama waweza tungani.
 
© boniphace Tarehe 1/17/2006 03:25:00 PM | Permalink |


Comments: 4


  • Tarehe 1/17/2006 7:28 PM, Mtoa Maoni: Blogger Jeff Msangi

    Msinisahau,nimeinama kama kobe vile,natunga sheria za maapisho.Nikirudi nitakuwa nimebeba bohora ili sote tukasheheni kuliko na sayari wasiyoenda wanadamu.Ushairi mzuri Makene,nasubiri majibu ya watani wako.

     
  • Tarehe 1/18/2006 2:29 AM, Mtoa Maoni: Blogger Ndesanjo Macha

    Makene na wenzako mmeleta msisimko mpya kwenye blogu. Mmekuja kwa nguvu hadi tuliokuwa ndani inabidi tuwapishe. Mwaka huu tutajua nani malenga mkuu.

    Jeff: neno 'bohora' limenisafirisha mbali.

     
  • Tarehe 1/18/2006 8:50 AM, Mtoa Maoni: Blogger mloyi

    Tungoye naiona
    makali nayasikia
    lughaye inachoma
    motowaka warudia

    Lughani
    kama ni ninii
    Motowaka siiwezani
    Kivulini najisitirini

    Yako maneno semezana
    Kunguru mfaona
    Nasubirina mzogao
    uwe wangu mlonaa

    Vita vya panzi
    afaidie kunguru.

     
  • Tarehe 1/24/2006 7:46 AM, Mtoa Maoni: Blogger Rashid Mkwinda

    Nawachia huu uga, Nyembo naye Makene,Najikita si kuaga katika tungo nene,zifundishazo kupwaga, mafundoye yaone.

    Bali bado ningalipo, Ulumbo sitawachia, nitalumba ipasapo, kuweka mambo sawia, Washindwao kwenye upo, elimu tawapatia.

    Kazi njema yaoneka, sote twaifurahia, Blogu yaneemeka,kwa mashairi kujazia, Wanablogu wasifika,ushairi ndio njia.

    Ushairi ndio njia, Kiswahili kukuzia,nahau misemo pia, methali kuzitongoa, Wa Ukuta na BAKITA, Blogu waje tembea.

    Waole tungo mahiri, hekima zilojalia,Zitongoazo urari na vina kupangilia.

    WAKATABAHU

     
   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved