Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Wednesday, December 28, 2005
SITTA SPIKA MPYA TANZANIA
KAMA utani hivi ndivyo imetokea hapo nyumbani Tanzania baada ya Spika wa miongo kadhaa Pius Msekwa kujikuta anaambulia aibu ya kushindwa kutetea kiti hicho. Alianza kama utani hivi miaka mitano iliyopita akiwahadaa wabunge kuwa hicho ni kipindi chaker cha mwisho, akadhani hawakumsikia, kisha juzi juzi akajitokeza tena kuomba nafasi hiyo, akisema Wabunge wamemuomba. Vyombo vya habari Tanzania vikaanika bila wazi na blogu nazo zikaweka bayana, ukawa mjadala mkubwa hali iliyoamsha ari ya kutazama mabadiliko na nafasi ya wengine katika utumishi wa umma.

Kuanguka kwa Msekwa kumetokana pia na makundi ya wazi yaliyomo katika chama cha Mapinduzi huku haya yakitokea tovuti ya CCM ilikuwa na picha zinazozunguka na moja ikiwaonyesha Rais Kikwete na Msekwa katika hali ya kuteta. Inaelezwa na wachunguzi wa masuala ya ikulu kuwa, Spika Mstaafu Msekwa aliomba nafasi kukutana na Rais Kikwete kuhoji kama analopendekezo lake katika nafasi ya Uspika. Hilo yaelezwa halikufanyika, lakini kundi lijulikanalo kama Wanamtandao, lililoongoza kampeni za uteuzi wa Kikwete, likiwa na mahasimu wakubwa wa Msekwa lilipinga wazi wazi kuteuliwa kwa Msekwa huku pia kundi lililokuwa likimpigia chapuo John Malecera likirejea tena na kumpigia chapuo Sitta na hivyo kujikuta mtandao wa Msekwa ukimong'onyolewa kama udongo mkavu utiwao maji.

Haya yanaanza kutokea wakati tayari Rais Kikwete amemrudisha bungeni Kingunge Ngombare Mwiru ikiwa ni katika viti anavyoteua Rais na hii ni moja ya zawadi kwa Kingunge kumuunga mkono Kikwete. Mfumo wa siasa za Tanzania saa chache zijazo utatazama jina jipya la waziri mkuu. Tayari picha imeanza kuonyesha kuwa awamu ya nne inaweza kutokuwa na jipya kufuatia misingi ya kubebana kuonyesha taswira ya awali kabisa. Majina mengine ya wabunge walioteuliwa na Rais Kikwete yanatabandikwa hapa baadaye.
 
© boniphace Tarehe 12/28/2005 09:08:00 AM | Permalink |


Comments: 3


  • Tarehe 12/28/2005 7:23 PM, Mtoa Maoni: Anonymous Anonymous

    Nimekupata kwa Miruko.Nimekumbatia kompyuta sasa kufungua blogu. Hebu pendekeza katika majina yale niliyokumegea kule Washington, DC lipi linafaa.

     
  • Tarehe 12/28/2005 9:31 PM, Mtoa Maoni: Blogger boniphace

    Nakaribisha hilo blogu kwa moyo wote. Ingia kaka tumekusubiri sana.

     
  • Tarehe 12/29/2005 12:58 AM, Mtoa Maoni: Blogger Fikrathabiti

    Mimi nadhani na huyu tumpe nafasi yake ila kama ujuavyo matumaini ya kuja na jipya ni madogo sana kwani amekulia katika mfumo kandamizi uliopo na kubadilika ghafla ni ndoto licha ya falsafa yake aliyokuja nayo ya "THE MAN OF STANDARDS AND SPEED"

    Halafu kaka makene kuna huyu mtu anaitwa Rostam Aziz mbunge kutoka Tabora anayesemwa kuwa na nguvu sana ndani ya CCM unaweza kunidokeza historia yake hasa uzoefu wake wa kikada ndani ya chama pindua?

    Yeye ndo alikua anatajwa sana kama kinara wa kampeni za Rais kikwete na ndo yeye tena aliyeongoza wanamtandao katika kuhakikisha bwana msekwa harudi bungeni na kumuunga mkono spika mteule.

     
   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved