Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Tuesday, December 13, 2005
NINI ISHARA YA HAYA

MGOMBEA wa urais na Rais ajaye wa Tanzania baada ya kura za kesho alianguka mapema jana wakati wa kukamilisha zoezi la kuomba kura. Wakati huu si kama ilivyokuwa Mwanza kwa kubebwa na gaidi mmoja lakini kwa sasa ni kile kinachozungumzwa kupungukiwa na nguvu baada ya kusimama wakati mwingi. Vyanzo vya habari hizi kutoka Marekani vilipasha tukio hilo huku vikilifananisha na jingine linalomkabili mgombea pekee Anna Senkoro, aliyefanikiwa kuweka rekodi ya kuwa muwania urais wa kwanza kabisa mwanamke Tanzania, ambaye hata hivyo hajapatwa kutajwa na DaMIJA katika blogu yake, kama alivyofanya katika makala hii na hii, naye tangu ngwe ya pili ya kampeni alikuwa kitandani kutokana na ugonjwa ulioambatana na kutoa hitilafu za mdomo wake na kukosa nguvu za kuzungumza.

Habari zadi za matukio ya aina hii yanatia kumbukumbu ya kifo cha mgombea mwenza wa CHADEMA aliyefariki mapema na kusababisha uchaguzi kuhairishwa. Hata hivyo habari za uchaguzi zinaonyesha hali ya mabadiliko katika nafasi za ubunge huku Kikwete akibaki kuwa Rais wa nne wa Jamhuri ya Muungano anayechukua nafasi katika kipindi kigumu kufuatia wigo kati ya maskini na tajiri kutanuliwa kwa spidi ya kawaida na serikali ya awamu ya pili huku hii ya tatu inayomaliza muda wake ikiwa imeongeza spidi na kufanya ufa huo kutotazamika.

Sera za Kikwete za ari mpya, nguvu mpya na kasi mpya zaweza kutanua ufa huo kwani yaonesha nguvu zake si kama alizokuwa nazo miaka kumi iliyopita. Pia anakabiliwa na makundi makubwa katika chama chake yanayotarajia fadhila kutoka kwake huku kukiwa na wengi wanaomsubiri kukalia kimya namna walivyojinufaisha kutokana na raslimali za umma.

Maskini wa Tanzania wanamuona Kikwete kama masiha mpya na wanahitaji kumuona akirejesha mali zao zilizobinafsisha kiholela huku sheria za ukandamizaji kama za kujiuzia mali za umma hasa nyumba zikifutwa na nyumba hizo kurejeshwa. Fikra hizi na nyingine nyingi huenda zimechangia kuanguka kwa Kikwete wakati wa ukamilishaji wa zoezi la kumfikisha huku alikoota kwa miaka mingi. Kuna habari nyingine ambazo nimezipata lakini zitaziweka sasa kwa sababu ya kiistaarabu.
 
© boniphace Tarehe 12/13/2005 09:52:00 AM | Permalink |


Comments: 4


  • Tarehe 12/14/2005 10:15 AM, Mtoa Maoni: Blogger Mija Shija Sayi

    Senkoro aja , Mwanazuo usishake,
    Hatosahaulika, kwa rekodi aloweka,
    Historia amekita, vitabuni imefika,
    Tulia Mwanazuo, Senkoro aja punde.

     
  • Tarehe 12/14/2005 4:02 PM, Mtoa Maoni: Blogger boniphace

    Nakushukuru Damija
    Nimeipata faraja
    Umekuja na kutaja
    Wazi utatimizia.

    Shairi umetungia
    Ubeti ukashibia
    Nami nakukariria
    shukrani kutolea.

     
  • Tarehe 12/15/2005 10:20 AM, Mtoa Maoni: Blogger Jeff Msangi

    Makene,
    Nadhani kuna haja ya AFYA ZA WAGOMBEA kuchunguzwa mara kwa mara hususani wakati wa pilikapilika za kampeni.

     
  • Tarehe 12/27/2005 1:48 AM, Mtoa Maoni: Blogger Fikrathabiti

    Mimi nadhani yaliyotokea yamefunua hali ya kutokua umakini kwa wasaidizi wa viongozi wetu wakuu wa nchi na ndo maana mtu akiugua mafua anaenda kutibiwa jijini kwa akina JEFF.

    Hivi kweli daktari wa huyu mheshimiwa mtarajiwa alishindwa kugundua udhaifu wa boss wake hadi alipoacha yatokee yaliyotokea???

     
   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved