Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Tuesday, December 13, 2005
KARIBU MALENGA MKWINDA
SI lengo langu kuhamisha mjadala ulioanzishwa na huyu jamaa baada ya kumtangaza Mwanablogu mpya huyu. Sijashawishika kutomchapa mwanablogu huyu malenga bakora za mashairi maana nimemisi majibizano haya tangu enzi zile nikiwa Ndanda Sekondari, wakati ambapo rafiki ya Shaaban Dammbaya aliweza kunipata hamasa ya kuandaa muswada wangu wa kwanza wa Mashairi ulioitwa "Hodi Hodi Duniani, Diwani ya Dammbaya na Nakuzerwa."

Nakumbuka maana kipindi hicho niliweza kukariri barua zangu kwa mashairi. Ni kipindi hicho nilipokuwa shabiki mkubwa wa Ustadhi Andanenga kabla sijakutana naye kwa macho pale Nkrumah Chuo Kikuu Dar es Salaam, katika usiku wa Ushairi nilipokuwa pia msema chochote huku nikighani tungo kama hizi;
Ya Liyongo hutwambia
Siu alikozaliwa
Pate akitembeleya
Na Mwana akafiliya.
Kutoka Utenzi wa Fumo Lyongo: ubeti huo unatangaza maisha yote ya Fumo Lyongo jasiri, shujaa katika upwa wa Afrika Mashariki miaka hiyo. Nakumbuka nilishokuwa nikiyapinga mapingiti ya Euphrase Kezilahabi lakini baadaye ni K. Kahigi aliyeweza kunibadili na kunirejesha kumuamini Kezilahabi na mtindo wao wa mashairi guni.

Hiyo ilikuwa chombeza tu lengo ni kumkaribisha malenga mpya huyu, kaja vema sana anapaswa kupongezwa kwa kujenga mhimili wa lugha katika Blogu. Kosa lake katangaza kitu ambacho nakumbuka napingana nacho katika beti alizojibu majibizano yangu na ghani ya maneno ya Ndesanjo.

Mkwinda kaka fikia, keti mwana bloguni
Zamani niliwazia, siku nitapokufani
Nani atashikilia, KASRI langu tunzani
Sasa napata faraja, kijana mpya tokea.
Umekuja kwa makeke, kisa changu kujibuni
Ulinifanya nicheke, machozi kinitokani
Vipi utaje mapene, kwa fani ya malengani
Mkwinda sasa useme, hisa unaziuzani?
Mapene wapi mizani, kitita sikitamani
Natunga nili zuoni, mapene kwangu sumuni
Siwezi kuyatamani, kwani yanageuzani
Utumwa wakumbukani, kisa mapene fatia.
Malenga vina pangia, hoja weka bloguni
Hatutaki majalia, ya pesa kutulipani
Ushairi nashibia, beti nazodondoani
Mkwinda acha makeke, ushairi si mapene.
Kalamu yake Ndesanjo, kali kaka ujuani
Wapaswa kukaa chonjo, Rais mtaniani
Utajatoa mkojo, Segerea laliani
Ndesanjo mtu mwingine, silinganishe na mimi!
Nimegundua kimoja, vina hujavipangani
Sasa niambie hoja, mapingiti watungani?
Kesho utakapokuja, tamka nikujuani
Kalamu ulofungua, wino imeshachojoa.
Tangu juzi nasemea, niko bize masomoni
Mitihani nafanyia, bado sijamalizia
Lakini mwatukania, kisa changu kujibuni
Kalamu nalaza chini, Mkwinda sigange njaa!
 
© boniphace Tarehe 12/13/2005 11:03:00 AM | Permalink |


Comments: 3


  • Tarehe 12/15/2005 4:20 AM, Mtoa Maoni: Blogger Ndesanjo Macha

    Mnanikumbusha mbali kweli. Kumbukumbu tamu sana hizi. Halafu nimefurahi umemtaja Fumo Lyongo. Twahitaji kuandika sana na kwa undani juu ya habari kama hizi maana hivi visa ndio urithi wetu (kama vile wayahudi walivyokusanya visa vyao kwenye torati na manabii). Ziko habari za akina Ngwanamalundi, kwa mfano.

    Turudi kwenye ushairi. Unanikumbusha enzi za kusoma gazeti la uhuru kila siku na kusikiliza RTD.

     
  • Tarehe 12/15/2005 4:37 AM, Mtoa Maoni: Blogger Ndesanjo Macha

    Tazama kiungo cha Mkwinda kina tatizo kidogo, umeweka "http" mara mbili.

     
  • Tarehe 12/21/2005 11:10 PM, Mtoa Maoni: Blogger FOSEWERD Initiatives

    Duuuuhhh sikujua na wewe ni mwanamalenga!! hongera sana bwana makene! Tanzania inahitaji makada kama wewe pia ili uchukue nafasi ya Tambalizeni! uwe tambalizeni wa kukomboa watu! sio yule mdidimizaji! - unajua ifike mahali kwamba shoka liitwe shoka na si vinginevyo! tusisifie hata vile vibovu! ndio matambalizeni wa zaza wa bongo walivyo!

     
   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved