Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Wednesday, December 21, 2005
ANALALAPI MIRUKO?
U wapi ndugu Miruko, zamani umepotea
Umenifanya kituko, nduguzo kuhadithia
Mbali umetupa mwiko, twakosa wa kupikia
Jamani nielezeni, Miruko amefikwani?

Mavitu nayatamani, mwezi sijayaonea
Labda ameshikwani, Keko ndani kaswekewa
Mgonjwa anawezani, mahututi kalalia
Jamani nielezeni, Miruko amefikwani?

Ya Kikwete na Nyerere, ya mwisho alitokea
Nilimtolea gere, kwa njia alopitia
Nikatamka tawire, kisa kipya pulizia
Kila nilipopitia, Miruko kanyamazia.

Nikajipa hamasiko, utulivu kachukua
Ni kosa lamba ukoko, kwa wazee najulia
Lakini kaka Miruko, Dodoma kalalia
Aha yawezekana, mwanamke kamwibia.

Nikapiga darubini, machinjioni onea
Suraye sijabaini, ni wazi amepotea
Polisi nikafikani, ripoti nikatolea
Nao wakanijibia, suraye hawajatiya!

Huu ni wito wa mwisho, bloguni andikia
Hapa sitaki michosho, mwapaswa mtafutia
Kama anaye kidosho, tujue apoishia
Siwezi kimya kalia, blogiye kusinzia.
 
© boniphace Tarehe 12/21/2005 09:28:00 AM | Permalink |


Comments: 3


  • Tarehe 12/21/2005 3:39 PM, Mtoa Maoni: Blogger Ndesanjo Macha

    Asante sana. Mimi nami nimekuwa najiuliza Miruko yu wapi? Majuzi aliniambia kuwa alipotea kutokana na pilikapilika za uchaguzi. Lakini safi sana "umempiga" shairi la nguvu. Wewe mashairi haya umeyahifadhi mfukoni ambapo unayachomoa kila dakika unayotaka au? Ustaadh, Malenga wa Kilwa sijui naye yu wapi.(namzungumzia: http://mkwinda.blogspot.com

     
  • Tarehe 12/22/2005 3:04 AM, Mtoa Maoni: Blogger Christian Bwaya

    Mimi ni msomaji wako wa siku nyingi katika blog yako, na gazeti la Mwananchi Jumapili. Unanitia changamoto sana Bwana Makene, hebu na tufahamiane sasa, au sio bwana?

     
  • Tarehe 12/22/2005 4:20 AM, Mtoa Maoni: Blogger mloyi

    Miruko mirukoni, nanga aipate
    bloguni haonekani,wapi nimpate
    nyumbaye vumbini,wadudu wapate
    dodoma ukumbini,kwake ajipate.

    Naingia kwake,naye haonekani
    ni nini kwake,kimyani akitani
    twasubiri yake,yeye hatupani
    kila sikuye,mlango hafunguwini.

    Ubaya hatuna,yake maneno matamu
    kuyakosa manona,yake yahamu
    habari hakuna,mafunzo hatujahitimu
    miruko yakuna,tupe wako ufahamu.

    Rejea ukumbini,nafasi yako iwazi
    tupate yako maoni,yaliyowazi
    mazuri usinyimani,mabayani utuwazi
    kwako mavituni,bado tunakuenzi.

     
   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved