Kasri, jumba la weledi waweza keti hapa na kupata ukitakacho. Chakula cha wakazi wa Kasri ni fikra na chakula hiki kimewapa thawabu wananchi wa nchi hii hali inayowafanya kutoziba midomo yao kila waonapo damu ya wanaonyanyaswa ikidondoka katika bahari ya dhiki, maangamizi na unyonyaji. Waweza nawe keti hapa na kula fikra hizi.
Wednesday, November 16, 2005
SAFARI YA MASHUA
NDUGU msomaji baada ya Mwanablogu mmoja kutoa kauli juu ya hili, nimpongeze kwanza nawe fanya hivyo kwa kumpa makofi kidogo, nimeanza na onyesho la kwanza. Nitakuwa nikichapisha mchezo huu wa SAFARI YA MASHUA ambao ni tamthiliya ambayo haikupata kutokea. Tamthiliya hii mpya inatungwa na kuhaririwa awali na Mwandishi Boniphace Makene na itachezwa kwa mara ya kwanza hapa katika Kasri hadi ikamilike. Ungana na mtunzi kutambua inahusu nini maana kuna jambo linalokuhusu sana hasa wewe mwanablogu wa Tanzania.

ONYESHO LA KWANZA

ANAONEKANA jamaa huyu ana wasiwasi hivi, anapita pale jukwaani kwa hadhari sana. Mkononi ana kalamu kama mbili hivi moja ina Manyoya hivi kama ile aliyokuwa akitumia Madson wakati wa mkutano wa kuandika Katiba ya Marekani. Amejikwaa chini, na ghafla umati unamzunguka. Unamtaka kuwahutubia lakini kabla hajafanya hivyo inatokea gari inayokuja kwa kasi na mara watu wote wanakimbia na kumuacha jamaa huyu aliyechana nywele kwa mtindo wa wei!

Anatembea na ghafla anakumbuka jambo, anakaa katika jiwe na kufikiri, jioni inamkuta hapo na kisha anaelekea ukingoni mwa Bahari. Pale kuna mvuvi mmoja. Huyu jamaa anamuomba na hao wanaonekana wakitweka tanga lao na kuingia baharini.

Jamaa huyu anaonekana kesho yake akiwa kafika Dar es Salaam mitaa ya Magogoni. Anatweta jasho huku sura yake chakavu sasa ina furaha. Ana makaratasi na sasa anaelekea ukanda ule wa bandari lakini kabla hajafika huko kuna gari linafika na kumchukua.

Huko kwao amesubiriwa kwa kitambo. Anawaza na ghafla anatoa makaratasi na kuandika, Anaandika, Makame, Rashid, Salim, Juma, Haji! Anayafuta tena hayo majina na kisha kutafuna hilo karatasi. Gari lile limemfikisha maeneo ya Kurasini na huko inapatikana mashua safi, yaonyesha iliandaliwa kwa ajili yake. Anapanda na kuondoa.

***********************************************************************************

KESHO YAKE MAENEO YA MJI MKONGWE

Upepo uliovuma jana katika mashua ulimfanya jamaa huyu kusahau kuwa karatasi alizokuwa kashikilia zilishalowana na wino ule uliotumika kuandikia uliyoyoma na maji. Hakuna maandishi katika karatasi hizi tena. Jamaa naona anatoka jasho na anaanza kujizungumzia mwenyewe.

Anakwenda Kusini, anageukia upande wa kuitazama Dar es Salaam. Anapaaza sauti na kuita Mabruuuki, Mabruuuki...anainama chini anaita tena Mama Amri, anachanganya majina sasa, Mama Ali, mama Zuwena, Husna, Juma...anaendelea kuita na kuita. Mwisho anaishiwa nguvu analala chini na kichaa mmoja mstaarabu anafika na kumchukua.

Anampeleka kwake, wapita njia wanashangaa kuona kichaa kufanya kazi hiyo. Wanatazama na baada ya kumfikisha langoni kwake kichaa yule anachukua kabisa yale mabaki ya maandishi yaliyoyolowa katika mashua, kichaa anakimbia, anaongeza kasi, anaenda na kasi zaidi. Ghafla anasimama akaribiapo bahari. Anapaza sauti na kusema, Wajingaaa..wajingaaa...wajingaaa
 
© boniphace Tarehe 11/16/2005 01:14:00 PM | Permalink |


Comments: 3


   
 
Copyright 2006 © BONIPHACE MAKENE. All Rights Reserved